| Hitimisho
Pepo ni makazi halisi ya Wanadamu, ni maisha halisi na ni mahali ambapo hapatakuwa na udhaifu wa kibinaadamu. Mwenye kunadi atanadi, mtakuwa na ubukheri wa afya wa milele, katu hamtaugua, mtakuwa na uhai wa milele, katu hamtakufa, mtakuwa na ujana wa milele katu hamtazeeka, na raha ya milele, katu hamtakuwa katika hali ya kutotosheka(Muslim). Qur'an inawaahidi Waumini kufaidi kukubwa na malipo yasiyokoma, na starehe za milele za maisha ya Peponi.
Peponi ni mahali pema pa maisha ya milele ambapo Allah (S.W) amepaandaa kwa malipo ya waja walioamini kama tulivyoona katika sura mbali mbali za kitabu hiki. Qur'an inaielezea kwa ufupi Pepo kwa kuyataja majumba ambayo watu wataishi humo, chakula watakachokula na vinywaji watakavyokunywa, nguo watakazovaa na vitu vizuri vizuri vitakavyokutwa humo. Tofauti na wengi wanavyodhani kuwa peponi kuna maisha ya kiroho, kwa hakika uhai na maisha ya Peponi, baada ya maisha ya ufu ya barzakh, ni wa maisha kama haya ya dunia bali yenyewe ni ya kudumu ni bora na halisi zaidi kuliko haya ya Dunia ambayo ni mchezo na starehe ya muda mfupi idanganyayo. Akiwa Peponi Mwanaadamu ataishi akiwa na umbile lake kamili bali lililobora zaidi ya hili alilonalo sasa. Maisha hayo ni mazuri mno yasiyostahili kulinganishwa na haya ya duniani licha ya kuwepo mambo yanayoonekana hufanana. Kutokana na mambo hayo, pale waumini wanapoyafariki maisha haya ya dunia na kwenda Barzakh kabla ya Akhera huwa hawapati hofu wala ugeni, hiyo ni kusema watayazoea maisha hayo kwa kukaribishwa na malaika na wenyeji wao vijana "Wildanu Mukhalladuuun" na wanawari waliotakasika "Hurun iin", hivyo watayazowea kirahisi tu. Maisha yao mapya ya milele yatakuwa kama yale waliyoishi hapa bali ya furaha isiyo na huzuni na ya starehe zaidi, kwahala ambako uchafu na uovu wote hautakuweko kabisa.
Kwa maneno mengine, watakuwa na vyakula na vinywaji bora, nguo maridadi kabisa, majumba mazuri, wake na waume. Kama isemavyo Qur'an, wataingia Peponi pamoja na wanawake ambao Allah amewazawadia kama malipo yao na watakaribishwa kwa shangwe na shamra shamra.
Ingieni bustanini Peponi nyinyi na wake zenu; mtafurahishwa humo (43:70).
|